Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Kumbukumbu ya Mwalimu Nyerere - Mara

HOSPITALI YA RUFAA MARA YAPOKEA MACHINE YA KISASA YA X-RAY

Posted on: April 14th, 2020

HOSPITALI YA RUFAA MARA YAPOKEA MASHINE YA KISASA YA X-RAY

 

 Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara, Leo imepokea mashine ya kisasa ya X-Ray (Digital X-Ray) kutoka Wizara ya Afya Maendeleo ya jamii Jinsia Wazee na watoto kwa ajili ya kurahisisha na kuboresha utoaji wa huduma ya   Mionzi katika hospitali za Rufaa nchini.

Akipokea mashine hiyo Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara Dr. Joachim Eyembe amesema kuwa,upatikanaji wa mashine hii ya kisasa kutaongeza ufanisi wa kazi kwa sababu machine hii ni bora Zaidi kuliko ile ya Analojia kwa kuwa ina uwezo wa kupiga picha zenye ubora wa hali ya juu na kuchunguza sehemu yeyote ya mwili wa binadamu.

Ameongeza kusema kuwa, mashine hii itasaidia  kwa kiasi kikubwa kuhudumia wagonjwa wengi kwa muda mchache kwa sababu  uwezo wake wa kutoa majibu ni muda mfupi takribani dakika kumi na tano(15), hivyo kwa siku ina uwezo wa kuhudumia wagonjwa mia moja(100).

Sambamba na hilo Dr.Eyembe ameishukuru serikali ya awamu ya tano  kupitia Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii,Jinsia Wazee na Watoto kuona umuhimu wa kuboresha huduma za afya  kwa kuleta vifaa tiba vya kisasa katika hospitali za Rufaa ambavyo vinasaidia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa huduma bora za  afya za wananchi.

Pia ameishukuru Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mara chini ya uongozi wa Mhe. Adam Kighoma Malima kwa kuwa mstari wa mbele katika kufuatilia na kuhakikisha upatikanaji wa huduma bora za afya pamoja na vifaa tiba katika Mkoa wa Mara unapewa kipaumbele na wananchi wa Mkoa wa Mara wanapata huduma bora za vipimo na matibabu.